Sunday, February 5, 2012

Three Crosses

Just a quick post. My homily for today's Sunday. In kiswahili language, so, please, use Google translator provided at the right sidebar of this blog to read in your native language...

Wapendwa waamini wenzangu,

Kila siku ya Dominika (Jumapili) tunaingia kanisani kushiriki Misa Takatifu. Na wengine wetu hata kila siku! Tunaadhimisha sadaka ileile ya Yesu Kristo aliyoitoa siku ya Ijumaa Kuu Msalabani. Sadaka ileile. Kuhani ni yuleyule, kafara ni ileile, matunda ni yaleyale. Siku ya Ijumaa Kuu Yesu alipanda Kalvario na kufa Msalabani. Padre anapanda Patakatifuni (ndo maana panajengwa mara nyingi kama mwinuko ili Kuhani akipanda ngazi ya Patakatifu ajue anakoenda na anaenda kufanya nini) na anarudia sadaka ileile ya Yesu japo kwa ishara za kiliturujia.

Ndugu zangu,

Katika kilima cha Kalvario cha Ijumaa Kuu, kulikuwepo na misalaba mitatu. Miili ya Yesu na ya wale majambazi wawili imekwishashushwa tayari karne ishirini zilizopita, lakini misalaba ile imebaki pale Kalvario hadi leo. Wengine sasa wanapandishwa. Wokovu umepatikana siku ya Ijumaa Kuu na siku ya Ufufuko wa Bwana, lakini Misalaba imebaki, mateso yako pale pale, maumivu yako pale pale, kifo kiko pale pale.

Tunapoingia kanisani kuadhimisha sadaka ya Yesu, sadaka ileile ya Ijumaa Kuu inayorudiwa katika Misa Takatifu, hatuna budi kuiona misalaba hiyo kwa macho ya imani. Kila mfuasi wa Bwana, awe ni Askofu, Padre, Sista, Bruda, Mlei – hana budi kuiona misalaba hiyo inaendelea kuwepo na kutusubiri pale pale Kalvario. Hatuna budi kuelewa kwamba sisi wenyewe hatuna uhuru wa kuamua tusulibiwe au tusisulibiwe. Mimi na wewe hatuna uhuru hata kidogo. Lazima nisulibiwe, maana mimi ni mkristo, na Yesu, Bwana wangu, ameniombea Msalaba siku ya Alhamisi Kuu alipomwomba Baba: „Baba, hao ulionipa nataka wawe pamoja nami popote nilipo, wapate na kuutazama utukufu wangu ulionipa” (Yn 17:24) Utukufu gani huo anaozungumzia Yesu? Ndio huu wa Msalaba: „Baba, saa imekwisha kufika. Mtukuze Mwanao, ili Mwana wako naye akutukuze wewe” (Yn 17:1) Kisha akasema: „Nami utukufu ule ulionipa nimewapa wao…” (Yn 17:22).

Basi, kama mimi ni mkristo kweli, kama kweli mimi ni mfuasi wa Yesu, sina budi kusulibiwa katika maisha yangu. Ndiyo hali yangu niliyorithi kwa wazazi wangu wa kwanza. Ndilo tunda la dhambi ya asili. Kwa Ubatizo niliondolewa laana ya milele, nikarudishiwa heshima ya kuwa mtoto mpendwa wa Mungu. Lakini athari nyingine zote anazozungumzia Mungu katika Kitabu cha Mwanzo, lazima nishiriki.

Lakini ninaweza kuchagua. Mbele yangu katika kilima cha Kalvario kuna misalaba mitatu. Natakiwa kuchagua moja. Nii juu yangu kuamua upi nichague. Nasi wakristo, kwa vile tunatofautiana sana katika mitazamo yetu kuhusu fumbo la msalaba katika maisha yetu, ndiyo maana tunatofautiana katika chaguzi zetu za msalaba.

Wengi wanachagua msalaba wa jambazi mbaya. Wanasulibiwa na wanamtukana Mungu. Wana mtazamo ule wa awali kabisa wa wazazi wetu wa kwanza ambao kwao msalaba, mateso, maumivu, shida, matatizo katika maisha yetu na hatimaye kifo ni vielelezo vya laana ya Mungu. Ni sehemu ya maisha yetu hapa duniani. Wakatoliki wengi tunabaki katika mtazamo huo. Tunakataa msalaba, tunakataa mateso na magonjwa, shida na matatizo, na vikitupata – tunalalamika, tunalipiza kisasi, tunahangaika na kujaribu kuepuka mateso kwa namna yoyote ile. Na tuko tayari hata kuingiza uchawi na ushirikina kama dawa ya matatizo yetu. Huo ni msimamo wa wapagani.

Wengine wanachagua msalaba wa jambazi mwema. Wanachagua njia ya kukubali tu mateso, kuvumilia mateso. Wanajisemea moyoni - ‘Kama nalazimika kupokea msalaba, basi, haya ndiyo ni mapenzi ya Mungu. Kubali yaishe’. Ndo mtazamo wa Ayubu: “Bwana alitoa, Bwana ametwaa, Jina la Bwana na libarikiwe!” (Ayu 1:21). Wanabaki kuvumilia na kumwomba Mungu awaondolee taabu hiyo wakitegemea mioyoni mwao kwamba hatimaye Mungu atawaonea huruma na atawapa tuzo kwa ajili ya uvumilivu huo katika mateso. Kama Ayubu ambaye amevumilia, na akarudishiwa mali zote, tena zaidi. Tunasoma katika sura ya mwisho ya Kitabu cha Ayubu: „Mungu .(…) akampa Ayubu mara mbili kuliko hayo aliyokuwa nayo kwanza (…) Basi hivyo Bwana akaubarikia huo mwisho wa Ayubu zaidi ya mwanzo wake: naye alikuwa na kondoo kumi na nne elfu, na ngamia elfu sita, na jozi za ng’ombe elfu, na punda wake elfu. Tena alikuwa na wana waume saba, na binti watatu (…) Katika nchi hiyo yote hawakuwepo wanawake waliokuwa wazuri kama hao wana wa Ayubu.” (Ayu 42:10b.12-13.15a) Ndio msimamo wa wakristo wengi sana tukiwemo na sisi wana Kiabakari. Tunadhani dhana hii ni sahihi. Sivyo. Huo ni msimamo wa Agano la Kale.

Msalaba wetu sisi wakristo ni huu wa katikati, alipokuwa amening’inia Yesu mwenyewe. Ndo zamu yetu kusulibiwa juu yake. Maana Yeye hafi tena, Maandiko Matakatifu yanavyosema! Mauti haimtawali tena. Ni zamu yetu – kuwepo pale alipokuwepo Yeye na kuonja utukufu ule ule.

Mkristo halisi hawezi kusulibiwa kwenye msalaba wa jambazi mbaya wala kwenye msalaba wa jambazi mwema. Itakuwa kituko. Mkristo halisi lazima asulibiwe juu ya msalaba wake ambao ndo Msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo.

Msalaba wa Yesu ni msalaba wa namna gani? Katika mtazamo wa Yesu Msalaba wake ni silaha ya kutisha. Nathubutu kutamka: Msalaba wa Yesu ni silaha ya maangamizo makuu ya yule mwovu, na wakati huo huo ni dawa bora ya kuleta wokovu kwa watu wa Mungu. Yesu alisema: “Mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele” (Yn 10:10). Alionyesha Msalabani alikuwa na maana gani! Msalaba wa Yesu si kifaa cha kumwangamiza Yesu kama ilivyokusudiwa na Shetani; si alama ya kushindwa kwake kuleta ukombozi duniani walivyodhani wengi; Msalaba wa Yesu ni mnara wa kumwezesha aone mateso yote ya ulimwengu na kuyakumbatia na kuyaponya. Akasema: „Naona kiu!” Si kiu chake, maana alikataa kunywa alipoletewa sifongo ya siki. Aliona, alihisi kiu cha vizazi vyote hadi kizazi chetu hiki. Ndo maana akasema: „Yeyote aliye na kiu, aje kwangu anywe!” Kisha akafungua ubavuni mwake chemchemi ya Huruma yake – damu na maji – alama ya miujiza miwili mikuu ya Huruma yake – Upatanisho na Ekaristi. Ndo maana mapadre wanapovaa stola – miisho yake miwili inakumbusha daima ni chemchemi gani zinapaswa kububujika kutoka ndani ya kilindi cha Ukuhani wao – Upatanisho na Ekaristi Takatifu - wapate kurudia maneno ya Yesu: „Nalikuja parokiani ili watu wa Mungu wawe na uzima, kisha wawe nao tele!” Hakuna chemchemi hizi popote pale pengine, ni katika Upadre tu. Padre mkatoliki ni umwilisho wa Huruma ya Mungu. Akikausha chemchemi hizi mbili ndani ya Upadre wake, asipoungamisha watu na kuadhimisha Ekaristi na kuwajenga katika imani hai na ibada kwa Yesu wa Ekaristi, watu wa Mungu basi ni wa kuhurumiwa mno! Vivyo hivyo sisi, wafuasi wa Bwana, tusipojenga maisha yetu ya kiroho juu ya Msalaba wa Kristo na chemchemi za Huruma yake katika sakramenti ya kitubio ya mara kwa mara na juu ya Ekaristi Takatifu, sisi pia ni wa kuhurumiwa mno!

Yesu aligeuza Msalaba wake, Mateso na Kifo chake kuwa silaha kali. Kutoka Msalabani aliona taabu za watu wote wa vizazi vyote. Akawasamehe makosa yao, akaanzisha Kanisa, akalifungulia chemchemi za uzima katika Damu na Maji toka Moyoni mwake, akaona kiu ya vizazi vyote, akapokea hisia zote za watu wake mpaka na zile za kukata tamaa, za upweke, za kila namna aliposema: Eloi, Eloi, lama sabakhtani?” Akamchukua jambazi mwema pamoja naye akiwa huyo ndiye wa kwanza aliyeonja wokovu wa Kristo na mpambe wa Yesu katika mlango wa mauti na hatimaye mbinguni; akatupatia Mama yake kama Mama yetu. Yeye mwenyewe aliamua muda wa kukamilisha sadaka yake, si kwamba aliishiwa nguvu au akakata roho kwa ajili ya kuteswa kupita kiasi. Maana Maandiko Matakatifu yasema wazi kuwa alipaza sauti kwa nguvu na kusema „Yametimia! Yamekwisha!” Nidpo akakata roho. Kumbe, si kwamba aliuawa, bali tungepaswa kusema kuwa Yesu alitoa kwa hiari yake na kwa muda wake sadaka yake msalabani na akaappoint saa tisa kuwa saa ya Huruma yake kwa vizazi vyote. Alifanya mambo mengi ajabu akiwa Msalabani. Wala hakuwa katika hali ya kuvumilia tu mateso, hakusubiri kifo tu; alikataa pia kishawishi cha kushuka Msalabani. Yesu alikuwa bize sana Msalabani.

Wapendwa waamini wenzangu,

Tujitazame sisi wenyewe. Je, kweli mimi ninapanda Kalvario kila siku kuadhimisha sadaka ya Yesu pamoja na kusulibiwa katika Msalaba wa Bwana wangu, ambao ni Msalaba wangu? Nikielewa kuwa ndiyo silaha ya kutuletea wokovu sisi sote?

Kuna Msalaba mmoja tu ulioleta wokovu kwa watu wa Mungu. Ndo Msalaba wa Yesu. Nao unapaswa kuwa wangu pia. Hali aliyoifikia Mt. Paulo, Mtume wa Mataifa, na kuieleza katika Nyaraka zake, hupaswa kuwa hali ya kila mmoja wetu, anapokiri: “Neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu.” (1 Kor 1:18) “Sisi tunamhubiri Kristo, aliyesulibiwa…ni Kristo, nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu.” (1 Kor 1:23.24) Na tena: “Lakini mimi, hasha, nisione fahari juu ya kitu chochote ila msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambao kwa huo ulimwengu umesulibiwa kwangu, nami kwa ulimwengu.” (Gal 6:14)

Ndugu waamini wenzangu,

Msalaba wa Kristo hutukumbusha kwamba hakuna upendo wa kweli bila mateso, hakuna zawadi halisi bila maumivu. Yesu baada ya Mateso na Kifo chake, akafufuka! Baada ya Ufufuko wake, hakuwa na muda kabisa na watesi wake tena, hakuwafuata, hakulipiza kisasi. Alikuja kwa watu wake tu na kujidhihirisha kwao kama Mfalme wa Huruma; akawapa amani, akawapa Roho Mtakatifu wa Upatanisho mara baada ya Ufufuko wake, akawauliza habari za upendo wao kwake kama sharti la msingi la kustahili kuchunga kondoo zake, hakuwa na muda kuwalalamikia kuwa walimkibia na kumwacha peke yake msalabani. Yesu anatuonyesha wazi maana halisi ya maneno haya.

Wapendwa waamini wenzangu,

Ninaamini kwa dhati kabisa kwamba katika maisha yetu, vipindi vya mateso, msalaba na majaribu mbalimbali vinavyotujia, mateso yasiyosababishwa na dhambi zetu sisi wenyewe, ni vipindi vyenye baraka kubwa mno ya Mungu. Ninathubutu kusema kwamba ni katika vipindi hivi hasa – tunakua na kukomaa katika Ukristo wetu kwa haraka zaidi na kusonga mbele kwa haraka zaidi katika safari ya wokovu wetu na wa watu wa Mungu. Nyakati za raha na mafanikio katika maisha yetu naziona kama pengine ningesema - half time tu, mapumziko tu kati ya vipindi vya msalaba, kama vile Mitume walivyopandishwa mlimani Tabor kuona utukufu wa Yesu wasije wakakwazwa watakapomwona Msalabani Kalvario. Nasi vivyo hivyo. Naamini kuwa Mungu – kama anatujalia mafanikio ya juhudi zetu, ni kwa ajili ya kutupumzisha tu, kututia moyo, kutuzawadia kwa hisia za kufanikisha jambo fulani na kutusaidia tukusanye nguvu mpya tuendelee na Msalaba wetu na kuzidi kukua kama wafuasi wa Bwana na makuhani wake. Ninaamini kuwa ofisi yetu kuu iko Kalvario, iko juu ya Msalaba wa Yesu. Kutoka hapo, katika mateso, uchungu na hisia za kuachwa na wote, hata na Mungu, katika mateso, katika jitihada zangu za kubeba hazina ya Ukristo katika chombo dhaifu ambacho ni mimi, ndipo ninapokuwa mfuasi kweli kweli kwa mfano wa Yesu.

Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uwongo, kwa ajili yangu. Furahini na kushangilia, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni!” (Mt 5:11-12). Naam, ndiyo maana tunapaswa kuwa na mtazamo wa Mt. Paulo aliyekiri: “Nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa Kristo ukae juu yangu. Kwa hiyo napendezwa na udhaifu, na ufidhuli, na misiba, na adha, na shida, kwa ajili ya Kristo. Maana niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu.” (2 Kor 12: 9b-10) na tena: “Nimejifunza kuwa radhi na hali yoyote niliyo nayo. Najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yoyote, na katika mambo yoyote, nimefundishwa kushiba na kuona njaa; kuwa na vingi na kupungukiwa. Nayaweza mambo yote katika Yeye anitiaye nguvu”. (Flp 4:11b-13) Na kwa njia hiyo kugeuza msalaba katika maisha yetu ya kikristo kuwa silaha ya kumwangamiza Yule Mwovu na kuleta wokovu kwa watu wa Mungu wanaotuzunguka.

Nawatakieni heri na mafanikio katika Utume wenu! Tumsifu Yesu Kristo!


No comments:

Post a Comment